Main Article Content

Uambatishaji wa Vishazi katika Lugha ya Kiswahili: Uchunguzi wa Madai ya De Vos na Riedel (2017)


Luinasia E. Kombe

Abstract

Makala hii inalenga kuchunguza madai yaliyotolewa na De Vos na Riedel (2017) kuhusu lugha ya Kiswahili kuambatisha vipashio visivyo na hadhi sawa. Miongoni mwa masharti ya uambatishaji ni mfanano wa kisintaksia wa vipashio vinavyoambatishwa (Chomsky, 1957; Lang, 1991; Munn, 1993; Johannessen, 1998). Kutokana na sharti hilo inaelezwa kuwa, ili kupata tungo ambatani inayokubalika kisarufi ni lazima vipashio vinavyoambatishwa viwe na hadhi sawa kisintaksia; yaani vifanane kikategoria na kidhima. Sharti hili la uambatishaji huchukuliwa kuwa ni majumui na hutumiwa kama kigezo cha kutofautisha utegemezaji na uambatishaji. Hata hivyo, De Vos na Riedel (2017) wanadai kuwa lugha za Kibantu, kikiwamo Kiswahili, hukiuka sharti hilo kwa kuwa zinaweza kuambatisha vipashio visivyo na hadhi sawa. Kwa kutumia Nadharia ya Sarufi Geuza Maumbo Zalishi, makala hii imebaini kuwa, tungo ambatani wanazozizungumzia wataalamu hawa katika lugha ya Kiswahili zimeathiriwa na kanuni za mageuzi. Kanuni hizo huzifanya tungo hizo zionekane kama zenye vipashio visivyo na hadhi sawa katika muundo wa nje, ilhali katika muundo wa ndani zimeundwa na vipashio vyenye hadhi sawa. Makala hii imebaini kuwa Kiswahili, kama zilivyo lugha nyingine ulimwenguni, huambatisha vipashio vyenye hadhi sawa. Data za utafiti huu zimekusanywa maktabani kutoka katika maandiko mbalimbali ikiwamo makala ya De Vos na Riedel (2017)1.

Journal Identifiers


eISSN: 0856-552X
print ISSN: 0856-552X