Main Article Content

Riwaya ya Kiswahili kama Tahakiki ya Jamii Baada-ukoloni


M Mbatiah

Abstract

Makala haya yanachukulia kwamba mwandishi wa Kiswahili haandiki tu kwa ajili ya kuandika bali huandika kukidhi mahitaji ya jamii anayoiandikia. Makala yanarejelea jamii pana ya Afrika Mashariki inayotumia lugha ya Kiswahili. Jamii ya mwandishi pia inaweza kuwa nchi mojawapo ya Afrika Mashariki. Tunatambua kwamba fasihi ya Kiswahili ina hadhira pana zaidi kwa maana ya kuwa inaweza kusomwa mahali popote ulimwenguni. Hata hivyo, mwandishi wa Kiswahili huilenga kwanza jamii yake. Hili ni jambo ambalo waandishi wengi wamekiri. Euphrase Kezilahabi, kwa mfano, amesema kwamba huwaandikia Watanzania, hasa wakulima wa mashambani.i Njia mojawapo ya mwandishi kutimiza matarajio ya jamii anayoiandikia ni kumulika kiini cha matatizo na uozo wa jamii inayohusika. Mwandishi hujaribu kujibu maswali kama vile: Kwa nini Mwafrika anatupa utamaduni wake na kuabudu Uzungu? Kwa nini mataifa huru ya Kiafrika hayawezi kujitegemea kiuchumi? Kwa nini maovu kama dhuluma, ufisadi na utawala mbaya yanazidi kuenea? Jawabu la maswali haya na mengine mengi, linahusiana na historia yetu, hasa kutawaliwa kikoloni. Waandishi wengi wa riwaya ya Kiswahili wanashughulikia athari hizi za ukoloni katika jamii zao. Hili ndilo suala ambalo makala haya yanajadili kwa kutumia data ya riwaya nne.

Journal Identifiers


eISSN: 0856-552X
print ISSN: 0856-552X