Main Article Content

Taswira ya Ulemavu wa Akili kama Mtindo wa Uzinduzi wa Jamii: Usawiri wa Mzee Gae katika Riwaya ya <i>Dunia Mti Mkavu</i> ya S. A. Mohamed


Beth N. Mutugu

Abstract

Makala hii inashughulikia matumizi ya taswira ya ulemavu wa akili kama mbinu ya uzinduzi wa jamii katika riwaya ya Dunia Mti Mkavu (1980) iliyoandikwa na Said Ahmed Mohamed. Kwa mujibu wa makala hii, ulemavu wa akili ni hali ya mtu kutokuwa na akili yenye urazini wa binadamu wa kawaida. Hali hii inadhihirika kutokana na mwonekano wa mtu, maneno na tabia zake. Matumizi ya mtindo huu yanalenga kuwasilisha maana halisi na mwafaka zaidi kwa uzito uliokusudiwa. Kama anavyosema Elran (2011), wahakiki wa kazi za fasihi wanapaswa kufahamu umuhimu wa taswira kama nyenzo ya kuwasilisha ujumbe kuhusu masuala mbalimbali yanayowakabili wanadamu. Makala hii imeangazia Mzee Gae, mmoja wa wahusika wakuu katika riwaya hii ambaye kwa mujibu wa wanajamii wenzake, anadhihirisha sifa za kuwa na ulemavu wa akili. Elran anasisitiza kuwa mwandishi anapotumia taswira fulani kama mtindo wa kuwasilisha ujumbe wake, anafanya hivyo kwa sababu mahususi. Taswira ya ulemavu wa Mzee Gae ni mfano wa namna ambavyo ulemavu wa akili unaweza kutumiwa na mwandishi kama mtindo wa kuwasilisha maudhui yake. Katika makala hii, Said Ahmed Mohamed amemsawiri Mzee Gae kama mhusika mwenye ulemavu wa akili. Hata hivyo, ulemavu huu unaibuka kama nyenzo muhimu ya kuwahamasisha wanajamii watambue hali ya dhuluma na unyanyasaji inayowazunguka ili waelewe kuwa kuna haja ya kuleta mabadiliko.

Journal Identifiers


eISSN: 0856-552X
print ISSN: 0856-552X