Main Article Content

Kuathiriana kwa Vipengele vya Kifonolojia na Kimofolojia katika Lugha ya Kiwanji na Kiswahili


Genoveva Mbilinyi

Abstract

Kuathiriana kwa lugha kumejadiliwa na wataalamu mbalimbali wakiwa wameegemea katika kuchunguza namna ambavyo lugha moja inaathiri lugha nyingine. Aidha, zipo tafiti chache ambazo zimezungumzia kuathiriana kwa lugha zikiwa na maana ya kupokezana kwa maathiriano ya lugha A kwenda lugha B na lugha B kwenda lugha A; mathalani, utafiti wa Mukuthuria (2004) ulichunguza kuathiriana kati ya lugha ya Kiswahili na lahaja ya Kitigania katika lugha ya Kimeru. Hata hivyo, kuathiriana huko kwa lugha kunatofautiana kati ya jozi moja ya lugha na jozi nyingine kutokana na upekee wa kila lugha kifonolojia na kimofolojia. Kwa hivyo, makala hii inalenga kuchunguza Kuathiriana kifonolojia na kimofolojia katika lugha ya Kiswahili na Kiwanji.Uchunguzi huu umetumia data iliyopatikana uwandani katika kata za Matamba, Mlondwe na Ikuwo wilayani Makete. Nadharia ya Uchanganuzi Linganuzi ya Lado (1950) ndiyo iliyotumika katika ubainishaji wa athari za Kiswahili katika Kiwanji na athari za Kiwanji katika Kiswahili. Matokeo ya makala hii inaonesha kuwa Kiswahili kimekiathiri Kiwanji na Kiwanji kimekiathiri Kiswahili kifonolojia na kimofolojia kwa watumiaji wa Kiswahili na Kiwanji.

Journal Identifiers


eISSN: 0023-1886