Main Article Content

Uhakiki wa Fonimu na Miundo ya Silabi za Kiswahili


Benard Odoyo Okal

Abstract

Fonimu ni kipashio kidogo cha sauti ya lugha chenye uwezo wa kubainisha maana na hudhihirika kama irabu au konsonanti. Kama ilivyo katika lugha nyinginezo ulimwenguni, Kiswahili vilevile kina fonimu za kategoria mbili yaani irabu na konsonanti. Hata hivyo, idadi ya fonimu konsonanti za Kiswahili inaelekea kuainishwa tofautitofauti kwa mujibu wa wanaisimu mbalimbali wa Kiswahili. Mathalani, wanaisimu wengine wanadokeza idadi ya fonimu konsonanti kuwa 24, 25, 26, 29, 32 au 33. Kwa upande mwingine, miundo ya silabi za Kiswahili pia hudokezwa kuwa tofauti kama vile 4, 5, 6, 7 na 8. Idadi tofauti ya fonimu konsonanti za Kiswahili pamoja na idadi tofauti ya miundo ya silabi za Kiswahili huelekea kuwakanganya wasomaji wa lugha ya Kiswahili. Hivyo basi, makala hii inalenga kuhakiki fonimu na miundo mbalimbali ya silabi za Kiswahili. Ili kufanikisha uhakiki huu, makala hii imehusisha katika upeo wake vijimada kama vile: dhana ya fonimu, uhakiki wa idadi ya fonimu za Kiswahili pamoja na mifano ya fonimu zenyewe. Makala imeshughulikia pia dhana ya silabi na uhakiki wa miundo ya silabi za Kiswahili. Uhakiki wa miundo ya silabi umeshughulikiwa ili kuangazia tofauti zinazodhihirika baina ya wanaisimu wa Kiswahili kuhusu idadi kamili ya miundo ya silabi za Kiswahili pamoja na mifano inayotolewa. Katika kujaribu kutanzua mgogoro uliopo, makala imerejelea kanuni zifaazo zinazoweza kutumiwa na mwanaisimu katika utambuzi wa fonimu na zinazotumiwa pia katika uundaji wa silabi.

Journal Identifiers


eISSN: 0856-552X
print ISSN: 0856-552X