Main Article Content

Ushairi wa Kiswahili kama Chombo cha Ujenzi wa Utangamano wa Kitaifa nchini Kenya


Joseph Maitaria
Clara Momanyi

Abstract

Makala haya yanafafanua dhima ya ushairi wa Kiswahili katika kujenga uwiano na utangamano katika jamii. Maendeleo na ustawi wa lugha huenda sambamba na fasihi yake. Ushairi wa Kiswahili kama utanzu wa fasihi, una historia ndefu. Aidha, umaarufu wa ushairi huu hautokani tu na vipengele vya lugha teule zinavyotumika, bali pia ujumbe muhimu unaowasilishwa. Hivyo basi, unaweza kutumiwa kama njia mojawapo ya kujenga utangamano miongoni mwetu. Kasi ya mabadiliko inayosababishwa na mchakato wa utandawazi imeufanya umma wa ulimwengu wa sasa kuangazia athari zake. Ongezeko la uhasama miongoni mwa jamii zetu, vita vya kikabila, tuhuma na ufisadi unaopaliliwa na ubinafsi, ni baadhi ya madhila yanayozikabili jamii za leo hususan katika eneo la Afrika Mashariki. Utangamano mzuri na maridhiano miongoni mwa jamii ni mambo ambayo hayana budi kuzingatiwa ili kuzikomoa jamii zetu kutokana na maovu haya. Katika mazingira haya basi, fasihi inakuwa chombo muhimu cha kujenga utangamano wa kijamii. Ushairi unaweza kutumiwa kama kioo cha kujitazama na kujisaili ili kujijengea ngome ya uwiano na utangamano katika jamii. Kwa mujibu wa muktadha huu basi, suala la utangamano wa kitaifa nchini Kenya linashughulikiwa kwa kurejelea utanzu wa ushairi. Baadhi ya mifano ya mashairi yanayoangazia suala hili inadondolewa ili kulipa uzito unaostahili. Aidha, makala yanaangazia baadhi ya vipengele muhimu vya kijamii ambavyo vinaweza kushughulikiwa kwa njia hii kwa lengo la kujenga ujamii na utangamano wa taifa.

Journal Identifiers


eISSN: 0023-1886