Main Article Content

Mkakati wa Tafsiri Mkopo wa Istilahi za Kiingereza katika Kiswahili na Athari zake: Uchanganuzi wa Vidahizo Teule vya Kamusi ya Biolojia, Fizikia na Kemia


Editha Adolph
Simon Chipanda

Abstract

Makala hii inachunguza mkakati wa tafsiri mkopo wa istilahi za Kiingereza katika Kiswahili na athari zake kwa kuangazia uga wa biolojia,  fizikia na kemia kupitia vidahizo teule vya Kamusi ya Biolojia, Fizikia na kemia (2012). Azma kuu ya uchunguzi huu ni kutathmini mchango  wa tafsiri mkopo wa msamiati wa Kiingereza katika suala zima la kukuza lugha ya Kiswahili. Kwa mujibu wa makala hii eneo hili  halijapewa aula miongoni mwa mada mbalimbali za tafsiri zilizokwishachunguzwa. Hii imemuhamasisha mtafiti kulishughulikia eneo hili.  Data ya makala hii ilikusanywa uwandani katika idara na taasisi zilizo katika jiji la Dar es Salaam kwa njia ya usaili, hojaji na chanzo cha  data cha maktabani. Idara na taasisi zilizohusishwa katika ukusanyaji wa data ni: Idara ya Lugha za Kigeni na Isimu, TATAKI kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam pamoja na BAKIZA. Idara na taasisi hizi zinapatikana mkoani Dar es Salaam Wilaya ya Ubungo ambapo mtafiti  alifanikiwa kudodosa na kufanya mahojiano ya ana kwa ana kwa wataalamu wa tafsiri. Aidha, data ilikusanywa kutoka katika matini  mbalimbali kutoka chanzo cha data cha maktabani. Mathalani, kamusi, tasinifu, majarida na vitabu kadhaa kulingana na mada ya makala  hii. Malengo ya makala hii yametimizwa kwa kuongozwa na Nadharia ya Istilahi za Kisayansi iliyoasisiwa na Kiingi (1989) na kuendelezwa  na Kiingi (1992) na Kiingi (1998) na Mwaro-Were (2000, 2001). Halikadhalika, data ya makala hii imechambuliwa kwa kutumia mkabala wa  maelezo. Aidha, matokeo yameonesha kuwa Kiswahili kimejipatia istilahi lukuki katika tasnia ya biolojia, fizikia pamoja na kemia kupitia  mkakati wa tafsiri mkopo. Makala hii ni muhimu kwa wanaisimu kwani inabainisha istilahi mbalimbali za lugha ya Kiingereza katika  uwanja wa biolojia, fizikia pamoja na kemia zilizoingizwa katika Kiswahili kupitia tafsiri mkopo. Inapendekezwa kuwa watafiti wa lugha  wachunguze njia nyinginezo za ukopaji zinazokiendeleza Kiswahili kama vile utohozi na uasilishaji.   


Journal Identifiers


eISSN: 2958-4914