Main Article Content

Sulubu bin Nguvumali, mhusika katika <i>Nyota Ya Rehema</i>: kigezo bora kwa Mtanzania wa Tanzania ya Viwanda


Masoud Nassor Mohammed

Abstract

Fasihi ni taaluma muhimu katika maisha ya binadamu wa zama zote. Taaluma hii humfuata mwanadamu kadiri ya mapito yake ya  kimaisha yanavyokwenda. Ni mwiko taaluma ya fasihi kupitwa na wakati. Tanzania ikiwa katika mkakati wa kufufua na kuimarisha  viwanda, fasihi ina mchango mkubwa katika azma hiyo njema kwa maendeleo ya Watanzania wote, wa vizazi vyote. Mchango wa fasihi ya Kiswahili katika maendeleo ya viwanda haupo katika mahitaji ya viwanda vya uchapishaji wa kazi za fasihi tu, haupo kwa viwanda  kuwasaidia na kuwahamasisha waandishi wa kazi za kubuni za kifasihi kupata fursa ya kuchapisha kazi zao tu, bali pia kwa namna ya  pekee kuchota mifano bora ya kuiga kutokana na baadhi ya wahusika wa kazi za fasihi ambao waandishi wetu wamewahi kuwasawiri katika sanaa zao. Makala hii inanuia kumuangazia mhusika mmojawapo wa kifasihi katika riwaya ya Nyota ya Rehema kama mfano sadifu wa kuigwa na kila Mtanzania katika wakati huu nchi ya Tanzania inapoimarisha viwanda. Mbinu ya uchanganuzi matini imetumika kuibua matendo mfano yatokayo ndani ya uhusika wa Sulubu katika riwaya ya Nyota ya Rehema iliyoandikwa na Mohamed Suleiman mwaka (1972). Makala imeonesha kwa uwazi namna mhusika Sulubu alivyokuwa mstari wa mbele katika mambo mablimbali: kupambana dhidi ya wanaokwamisha maendeleo, kutoa elimu sahihi ya kilimo, kufahamu hali ya soko na mahitaji yake, kujikita katika ufugaji, kufanya kazi kwa bidii bila kukata tamaa pamoja na kuimarisha mashamba ambayo yalionekana hayafai kwa kilimo kama ambavyo Serikali ya Tanzania inavyofufua viwanda vilivyokufa kwa muda mrefu. Kutokana na matokeo ya utafiti huu, makala hii ni muhimu kwa wananchi, wasomi na taifa la Tanzania kwa ujumla. Inaamsha ari ya Watanzania kufanya kazi kwa bidii ili kufufua na kuvilisha viwanda vya Tanzania malighafi zitokanazo na juhudi ya kazi zao wenyewe.


Journal Identifiers


eISSN: 2591-7013
print ISSN: 2665-0789